Ijumaa, 9 Mei 2025

MAPENZI HAKUNA!

Nina jingi jakamoyo, linonipiga katiti

Kulitowa kwenye moyo, yabidi nijizatiti

Maana kwa wengi siyo, wana nyingi ati ati

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


Pendo usiliasisi, ukaliona ni fiti

Mwenye nalo yuna nuksi, huweza kukusaliti

Ni ndugu zake Yudasi, na wanazo ithibati

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


Moyo una nyingi siri, kingi kizungumkuti

Uahidiwe sayari, na nyama kwa sharubati

Kwenye ndoto utajiri, siwe mwepesi kubeti

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


Wengi wana nia zao, na njama za kukuseti

Ukishatekwa na wao, ushindwe kujithibiti

Mwisho ukapinda tao, na kujikuta maiti

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


“Kimwana umerembeka, wawaka ja kiberiti

Nakupenda ni hakika, nina nawe mikakati”

Hayo mafamba epuka, utapigwa mabaluti

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


Yapo mengine mabusu, kama ya Iskaryoti

Alivyofanyiwa Yesu, kauzwa senti thalati

Lahitaji udurusu, penzi la kupigwa goti

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


Kwa hili fungu la saba, ndipo nakomesha beti

Penzi ni kama msiba, ukishatendwa na switi

Moyo utakosa tiba, onyo la bwana Sereti

Hakuna penzi la dhati, sihadaiwe na mtu!


© Limehaririwa Jumanne 25.02.2025