Jumapili, 11 Mei 2025

PONGEZI MAMANGU!

Kutunga ni yangu haja, nisifu mama mzazi

Leo mama nakutaja, tena nikupe pongezi

Ukanizaa miuja, tumboni kenda miezi

N’ambie tunu azizi, nikampe mama yangu!


‘Linifanyia natija, nivaazo na malazi

‘Kanipikia mrija, kunywa uji kwa viazi

Tena ukanipembeja, niupate usingizi

N’ambie tunu azizi, nikampe mama yangu!


Nilipolia ukaja, kunitolea tatizi

‘Kanipapasa mapaja, kunilaza kwa ujuzi

Ukaniimbia luja, nilipokosa tulizi

N’ambie tunu azizi, nikampe mama yangu!


‘Kanijengea daraja, nisome nikamaizi

Leo Napata faraja, najua zile na hizi

Mama napanga lahaja, zizi hizi kumbukizi

N’ambie tunu azizi, nikampe mama yangu!


Sitasema ngojangoja, kukufidia mzazi

Mimi nawe kwa pamoja, ndimi wako mtetezi

Nijapokupa korija, ninaona sikujazi

N’ambie tunu azizi, nikampe mama yangu!


Nipasulie viroja, kama wataka ghawazi

Nitimie niwe mja, mama, nikupe Feruzi?

‘Takujazia mkaja, chapati na maandazi

N’ambie tunu azizi, nikampe mama yangu!



**************************************

(Utunzi wa: Sereti M. Nema, Malenga wa Msituni, Diwani ya Uzindushi, 2009).

Kumbukumbu kwa Sikukuu ya Akina Mama, japo mama aliaga dunia Januari 14, 2024, daima nitadumu kumshukuru kwa kunizaa, kunilea na kunifundisha.

Jumapili 11 Mei, 2025.


#HAPPYMOTHERSDAY

#MyMotherMyHero

#Kisiki