Nimechoka tangatanga, kila tengo nimefika!
Mithili mtu mjinga, vizuri asojiweka!
Yamenifinya majanga, utumwani kuteseka!
Kurudi kwetu nataka, duniya imenisonga!!!
Duniya imenisonga, kurudi kwetu nataka!
Kwa nini nilijitenga, na watu walosifika?
Kwangu huku kutochunga, kumenileta mashaka!
Kurudi kwetu nataka, nimekonda sina hali!!!
Nimekonda sina hali, kurudi kwetu nataka!
Hata usiku silali, naumu zimen'toweka!
Mavazi sina sijali, kufa nani anataka?
Kurudi kwetu nataka, nani atanikubali?
Nani atanikubali, kurudi kwetu nataka!
Chawa wamenikabili, damu yangu waitaka!
Kila mtu hanijali, viumbe vyanitoroka!
Kurudi kwetu nataka, ugenini kuna dhiki!
Kweli nimeisha hamu, narudi kwetu nyumbani!
Yamenichusha magumu, nilopata ugenini!
Nusura nife Kisumu, kwa maradhi kitandani!
Hata kama pawe duni, nyumbani kweli patamu!
Ola nilivoduwaa, sina wa kuniauni!
Hata nikiwa kazini, kamwe sikufurahia
Hata hivyo kazi gani, pato wanakukatia?
Sitaki kufanya deni, nianze kufatilia!
Nyumbani ni nyumbani tu, hata kama ni chooni!
Siku nzima shinda njaa, pesa huna mfukoni!
Hata nikawe shujaa, magonjwa yapigwe nini?
Narudi kwetu nyumbani, ugeni sitakaa!
DIWANI YA MRATIBU, 2013.
Huu ndio mtandao wa kipekee utakaowaauni wapenzi na wakereketwa wa lugha ya Kiswahili. Nimeubuni ili kukuza kipawa, usanii na utamaduni. Utaasika, udadisi na licha ya kuelimika, utaburudika. Usikose kuniachia ujumbe wako, ili nami nijielewe. Asante na karibu.
Jumatano, 14 Agosti 2013
GUGUMAJI (IBILISI MREMBO)
Ziwani linabishana, na samaki ufukweni!
Kwa kasi kuzaliana, bali halina thamani!
Sura huvutia sana, ndani maficho ya jini!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
Limenitenda kichuna, zogo na purukushani
Usiku hata mchana, sina furaha moyoni
Kufyeka na kuvutana, tabia za kishetani!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
Juu maji 'kiliona, ni uwanja wa kijani
Chini maji yajazana, kukuhadaa machoni!
Vijinyama vimechina, kukosa okisijeni!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
Kwa urembo limefana, bali vitendo ni duni!
Kwanza nilipoliona, nilihisi burudani!
Bali uhai halina, lafisha kama tufani!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
Mmea huu mpana, na mingine hufanani!
Kwenye maji hapa mbona, unapataje madini?
Siutaki naukana, wavuvi tu vilioni!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
Wataishi vipi ngwena, na samaki mashakani?
Nasi ndo yetu hazina, kwa wenyeji na wageni
Madau, meli, safina, hazipiti abadani!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
Nani atapatikana, asiliye abaini?
Gugumaji kulichuna, viumbe kuviauni
Nema kichwa najikuna, nirudipo Msituni!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!
DIWANI YA "MRATIBU", 2013.
Jisajili kwenye:
Machapisho (Atom)