Jumatano, 14 Agosti 2013

GUGUMAJI (IBILISI MREMBO)


Ziwani linabishana, na samaki ufukweni!
Kwa kasi kuzaliana, bali halina thamani!
Sura huvutia sana, ndani maficho ya jini!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

Limenitenda kichuna, zogo na purukushani
Usiku hata mchana, sina furaha moyoni
Kufyeka na kuvutana, tabia za kishetani!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

Juu maji 'kiliona, ni uwanja wa kijani
Chini maji yajazana, kukuhadaa machoni!
Vijinyama vimechina, kukosa okisijeni!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

Kwa urembo limefana, bali vitendo ni duni!
Kwanza nilipoliona, nilihisi burudani!
Bali uhai halina, lafisha kama tufani!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

Mmea huu mpana, na mingine hufanani!
Kwenye maji hapa mbona, unapataje madini?
Siutaki naukana, wavuvi tu vilioni!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

Wataishi vipi ngwena, na samaki mashakani?
Nasi ndo yetu hazina, kwa wenyeji na wageni
Madau, meli, safina, hazipiti abadani!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

Nani atapatikana, asiliye abaini?
Gugumaji kulichuna, viumbe kuviauni
Nema kichwa najikuna, nirudipo Msituni!
Nimepata nilidhani, kumbe nimepatikana!

DIWANI YA "MRATIBU", 2013.

Maoni 1 :