Jumatano, 21 Agosti 2013

HONGERA KISURA!

Nema naja jukwaani, kuikatisha subira!
Niseme yalo moyoni, tuloshushiwa ghufira
Nipokeze shuqrani, shule'etu kutia fora!
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Wahitaji shuqrani, Tabitha wetu kisura
Matokeo ya mwakani, tukapata kumi bora
Siwavalii miwani, walimu wetu hongera!
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Ulotenda mhisani, shuleni siyo hasara
Mikataba kusaini, vitabu tukavidara
Kapita madarasani, ukapeana busara
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Makelele vidatoni, walokuwa kuzurura
Walopoteza imani, wote kawapa tijara
Akaziweka kanuni, zikasimama imara!
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

 Makelele vidatoni, walokuwa kuzurura
Walopoteza imani, wote kawapa tijara
Akaziweka kanuni, zikasimama imara
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Toka juu hadi chini, aliunganisha dira
Walimu wa afisini, wakatuvunjia nira
Tukaingia vitani, tukaacha masihara
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Wazazi waliamini, wakavaa matambara
Mwana aende shuleni, kujiundia ijara
Leo tupo shereheni, wazazi wetu hongera!
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

 Vitabu maktabani, na kujengwa maabara
Ni mwanzo wa tumaini, kujaliwa madhukura
Tuingie masomoni, tuitimize ishara
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Asante wetu wageni, mumetujaza fikara
Kupita ni letu deni, nawaombea subira
Sikusahau Diwani, Bibao George Morara
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

Wanafunzi jikazeni, msije mkatukera
Muingie vyuoni, tufukuze ufukara!
Kerongorori jamani, siku zote tukang'ara!
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

 Malenga wa Msituni, niwapokeze taswira
Mwaka huu hamsini, watafata taashira
Mola utupe hisani, tufyatuke ja kombora!
Bibi Tabitha hongera, uongoze shule yetu!

KWA MWALIMU MKUU,
BI. TABITHA MOGONCHI,
SHULE YA MSETO, KUTWA NA MALAZI - UPILI, KERONGORORI.
(Shairi hili, nililitunga na kulighani nikiwa mwanafunzi kidato cha nne, katika sherehe SIKUKUU YA TUZO, Mei 15, 2009).

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni