Wapo wanaotafuta, wa kumpenda hawana!
Wewe ndiwe nilipata, maishani kupendana
Ashiya wa bukhrata, hatima ya kukutana
Ingawaje mali sina, mpenzi, nakupa moyo.
Usiyependa maringo, majigambo wewe huna
Umbole la mviringo, alilokupa Rabana
Una ya upanga shingo, nywele zilizojichana
Mrembo wangu Regina, mpenzi, nakupa moyo!
Sura yako afya kwako, hata ujipake hina
Roho ya mtu iliko, ndiko kwenyeye hazina!
Nema nimetuwa kwako, azizi Wango Regina
Nitakachokupa Nana, Mpenzi, nakupa moyo!
Kila mara nakuwaza, usiku hata mchana
Ndiwe ninayetukuza, bila wewe raha sina
Usije kunipuuza, mpenzi sinitukana!
Kusudi kutulizana, Mpenzi, Nakupa moyo!
Kila mara nakuwaza usiku hata mchana
Ndiwe ninayetukuza, bila wewe raha sina
Usije kunipuuza, mpenzi sinitukana!
Kusudi kutulizana, Mpenzi, Nakupa moyo!
Wango kito cha thamani, ni wewe mwengine sina
Nipe raha maishani, tuishi tukipendana
U malaika wa shani, huna wa kumfanana!
Umenipendeza sana, Mpenzi, Nakupa moyo!
Mwisho nanga naitia, kukuimbia Regina
Leo nakufichulia, Nema nakupenda sana!
Tuhifadhi yetu ndoa, Mola akatupe wana!
Mimi nawe twatoshana, Mpenzi, Nakupa moyo!
KWA MKE WANGU MPENDWA,
REGINA WANGO NEMA,
"KUMBUKUMBU ZA NDOA YETU - MIAKA MIWILI"
Julai 17, 2012.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni