Jumatano, 21 Agosti 2013

SIKU YANGU

Ningekuwa na mabawa, kama ndege ningeruka
Nifike kwenye maziwa, penye misitu na nyika
Kumshukuru Moliwa, aloniongeza mwaka
Mwakani naikumbuka, siku niliyozaliwa!

Shaabani ilikuwa, themanya-sidusi mwaka
Ishirini-tatu chwewa, mapema kupambazuka
Fatiha ikajibiwa, myezi kenda kutimika
Mwakani naikumbuka, siku niliyozaliwa!

Nisaidieni njiwa, makero kutambilika
Swala njema kuombewa, kwa khatwiri ya shufaka
Mema piya kutakiwa, nyoyonimwe wahibaka
Mwakani naikumbuka, siku niliyozaliwa!

Vinono nikichinjiwa, siwezi nikaridhika
Dengeluwa kujaziwa, na keki za kubanika
Nishirikishie duwa, kwa Mola na malaika!
Mwakani naikumbuka siku niliyozaliwa!

SHEREHE ZA KUADHIMISHA MWAKA WANGU WA 25.
KWA WAPENZI WANGU WOTE WENYE NIA NJEMA NA DHAMIRI.

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni