Kazi yangu ya mikono, ndugu nishapowambia
Ni mshipi wa kiuno, nitakapojifungia
Mbona yenu minong'ono, pote mnapotembea?
Mbona mnajisumbua, nifanyapo kazi yangu?
Finyango nazofinyanga, Mola amenijalia
Mbona msipojitenga, matusi mwanitupia?
Kwa nini mnanipinga, mwanisengenyea pia?
Mbona mnajisumbua nifanyapo kazi yangu?
Wema tenda zako nenda, wahenga walitwambia
Yenu mnayoyatenda, ni nani mtagaia?
Kazi yangu nayopenda, mbali mwaitupilia!
Mbona mnajisumbua, nifanyapo kazi yangu?
Kama mngekuwa wema, auni kunichangia
Mnipe busara njema, nami ningewaungia
Sasa mwaipanga njama, mwataka kuniulia!
Mbona mnajisumbua, nifanyapo kazi yangu?
Mmenisumbua sana, mori imenipandia
Sipendi kufarakana, na watu wasio njia
Mwajifanya mnaona, hamnazo kujitia
Mbona mnajisumbua, nifanyapo kazi yangu?
Kaditama wa tamati, utunzi kumalizia
Hela nenda jizatiti, kazi zenu jifanyia
Naitwa Nema Sereti, ujumbe nawatilia
Mbona mnajisumbua, nifanyapo kazi yangu?
DIWANI YA "UREMBO WA NEMA, 2003".
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni