Jumapili, 11 Agosti 2013

BIN-ADAM

Nina kauli-kinzani, peupe naianika!
Ituhusuyo insani, na sifa tunojivika
Majigambo midomoni, mwenzi-kwa-mwenzi mipaka!
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

Tajiri na masikini, wapi wote walitoka?
Kujigamba na mapeni, jumba, gari, madaraka!
Mkata mwenye huzuni, isitoshe wamcheka!
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

Nayaingilia ndani, naomba kueleweka!
Unapoenda bafuni, kukoga ukasafika
Wapangusa maungoni, na marashi kujipaka
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

Urembo wako mwilini, aliokupa Rabuka
Unakufanya huoni, wengine ni takataka!
Usifanye uhaini, mawaidha kutapika
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

Ningeishi mawinguni, ningekuwa malaika!
Kuliko ulimwenguni, huku kulikochafuka!
Mtu ni utu jamani, bure unachacharika!
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

Towa nta sikioni, binadamu msifika
Alotuumba Manani, duniani katuweka
Pua zyangalie chini, na ndipo tulipotoka
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

 Nenda zangu Msituni, nikiwa nimeudhika
Bali furaha moyoni, kwa ujumbe kunitoka!
Sote tujivishe soni, ja nguo zimeraruka!
Kama u safi, taulo, inachafuka kwa nini?

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni