Jumapili, 11 Agosti 2013

SILI NYAMA YA NGURUWE!

Sili nyama ya nguruwe, leo nimeitambua!
Nimeikana mwenyewe, bila mtu kunambia!
Inanitia kiwewe, pia inanichafua!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Silazii nipikiwe, mboga zijapokosea
Hamu isinizuzuwe, zama nikikumbukia
Muwele sitaki niwe, nilokula yatoshea!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Nilisoma nimwelewe, kwa nini twamchukia!
Mola hataki aliwe, Qur'ani na Biblia
Mbali akatupiliwe, alipo kupakimbia!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Wacha mbwa wapikiwe, wao watafurahia!
Sitaki nipambaniwe, Jehannam n'kaingia
Na kwangu asifugiwe, sina chembe ya hisia
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Harufu yake nguruwe, pote anapopitia
Ataka mumtambuwe, msipomuangalia
Ni benibeni mwendowe, tapishi kwake halua!
Ni nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Ni vyema nikashifiwe, na wenzangu familia
Wala cheo nisipewe, kundi kulisimamia!
Bali kufuga nguruwe, nimekana niachia!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Kwa mafuta asifiwe, na juhudi kitabia
Kila kitu akijuwe, anuse na kujilia
Atamani mbele awe, kwanza mapya kupokea!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Watalii wachinjiwe, uchu kuwaondolea!
Filamu wachukuliwe, wa ng'ambo kupelekea!
Ama mbwa wapikiwe, na punda kufurahia!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Kitambo niing'wafuwe, sikuwa nimeijua!
Sasa leo iepuwe, ni haramu nisikia!
Mara ngapi muambiwe, kwamba ni mbaya! Yaua!
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Yanipa maruweruwe, ijazwapo sufuria!
Nashindwa vipi iliwe, na mbwa waingojea!
Ninakoma nipumuwe, ujumbe huu pokea:
Ni 'nyama mwenye udhia, sili nyama ya nguruwe!

Hakuna maoni:

Chapisha Maoni