Moyoni nimeumiya, nimepagazwa kupenda
Juhudi nilizotiya, tiarangu kuiunda
Hewani kuitezeya, na upepo ikaenda!
Kukosa ulichopenda, rahisi kukichukiya!
Angani ilipo'ngiya, eneole ikatanda
Uzi nikaachiliya, 'kadhani itajipinda
Nyuma kuifatiliya, tiara 'kazidi kwenda!
Kukosa ulichopenda, rahisi kukichukiya!
Wapi imepoteleya, tiara niliyopenda?
Vipi nitaifikiya, na kupaa kwanishinda?
Ni hofu kuvumiliya, na jinsi nilivyokonda!
Kukosa ulichopenda, rahisi kukichukiya!
Mlo nazo 'sinambiya, nimeapa kutopenda!
Tiara zina kayaya, kupozi nazo kwa inda!
H'wenda ikawa kinaya, dhidi ya pepo 'zilinda!
Kukosa ulichopenda, rahisi kukichukiya!
Ahsante sana hewala, kwa auni za busara!
Nilikuwa nimelala, nikiwaza kwa hasira
Bali nasema Inshalla! Nitaipata tijara!
Nilomsifu "Tiara", kwangu ameshakugura!
Pishi nashindwa kulila, pendo halina sitara
Chumba tulopamba sala, nakiona ja ahera
Mola ukiwa ni hila, nipe mwengine kisura!
Nilomsifu "Tiara", kwangu ameshakugura!
Nimelingana kwa Mola, atujeze maghufira
Apate alo aula, nami nimpate bora
Mambo yasiwe ghafula, huvuta heri subira!
Nilomsifu "Tiara", kwangu ameshakugura!
DIWANI YA MRATIBU, 2013.
Hakuna maoni:
Chapisha Maoni