Jumapili, 11 Agosti 2013

NYOTA YANGU

Nyota yangu ya thamani, nahitaji kukuona
Umenikaa moyoni, bila wewe sitapona
Wapotelea gizani, ninapolala kichuna!
Nyota yangu ya usiku, nakutamani mchana!

Nimeshindwa kutulia, na imenikumba suna
Usiku kukungojea, nguvu za kukesha sina!
Ghafula ninasinzia, kwa usingizi wa kina
Nyota yangu ya usiku, nakutamani mchana!

Mchana nina nafasi, mie nawe kuonana!
Tujilaze kwenye nyasi, ya moyoni kuyanena
Twondowane wasiwasi, mawazo kutulizana!
Nyota yangu ya usiku, nakutamani mchana!

Mwangaza wako wa shani, wanijaza uchu sana!
Ndio ninaotamani, kwenye anga la mchana
Nakuomba niauni, nyota yangu ya maana!
Nyota yangu ya usiku, nakutamani mchana!

Giza linapoingia, wenzi wananitukana
Shere wananifanyia, ndoto yangu kuibana
Bali nitavumilia, madhali tunapendana!
Nyota yangu ya usiku, nakutamani mchana!

Kigae cha almasi, uso uliojipuna
Nakomea hapa basi, nimejua hutanuna!
Ushindane na shamsi, usiku ung'ae tena!
Nyota yangu ya usiku, nakutamani mchana!

Maoni 2 :